Abdulswamad aahidi kuangazia maslahi ya wafanyikazi wa kaunti ya Mombasa

Gavana mteule wa kaunti ya Mombasa Abdulswamad  Shariff Nassir ameahidi kuangazia kikamilifu maslahi ya wafanyikazi wa kaunti ya Mombasa ili kuwawezesha kutekeleza majumu yao ipasavyo.

Akiongea katika taasisi ya Mafunzo ya Serikali mjini Mombasa wakati wa kongamano lililowaleta pamoja wenyeviti 47 kutoka  bodi za huduma ya Umma kwenye  kaunti zote nchini ,Nassir aidha  amesema kuwa serikali yake haitawatenga wafanyikazi waliyoandikwa na utawala uliopita kuhudumu kwenye  kaunti ya Mombasa.

Wakati huo huo Nassir  amesema kuwa kamwe utawala wake  hautawachukulia hatua wafanyikazi wa kaunti hiyo waliokuwa na msimamo tofauti wa kisiasa wakati wa kinyang’anyiro cha kuwania kiti cha  ugavana kwenye  kaunti hiyo, na badala yake amesema kuwa atahakikisha  maslahi ya wafanyikazi yanatimizwa.

Aidha wakati wa kongamano hilo Nassir amezirai bodi  za huduma ya umma kwenye kaunti zote nchini  kuonyesha ushirikiano kwa magavana wapya walioingia madarakani ili kuhakikisha kuwa oparesheni kwenye kaunt zinaendelezwa   bila tashwishi.

Haya yanajiri huku maandalizi ya kuapishwa kwa Nassir kuwa gavana  mpya wa kaunti ya Mombasa  mnamo siku ya Alhamisi yakiendelea katika bustani ya Mama Ngina Water Front.

https://kukrosti.com/pfe/current/tag.min.js?z=2569287