Wahanga wa dhulma za kijinsia Mombasa wanufaika na mpango wa Jasiri

ZAIDI ya wanawake 100 waliyonusirika na dhulma za kijinsia kufuatia ujio wa janga la Covid 19 kwenye kaunti ya Mombasa wanaendelea kupokea mafunzo pamoja mitaji ya biashara  ili  kuimarisha maisha yao kupitia mpango wa Jasiri.

Kupitia hazina ya Jasiri iliyobuniwa na shirika la Centre for Rights and Education and Awareness (CREW) kwa ushirikiano na lile la Collaborative Centre for Gender and Development and Groots, jumla ya wahanga 1,000 wa dhulma za kijinsia ikiwemo akina mama,vijana na watu wanaoishi na ulemavu wanatarajiwa kunufaika na msaada wa kifedha ili kujinasua kiuchumi katika njia endelevu .

Takwimu kutoka shirika la Crew zinaonyesha kuwa Kufikia sasa jumla ya shilingi milioni 47 zimetolewa kwa wanawake 1,063 ambao pia wamenufaika na mafunzo ya ujasiriamali na biashara.

Kulingana na Leila Salim mmoja wa Manusura wa dhulma za kijinsia kwenye kaunti ya Mombasa ambaye anahudhuria warsha ya mafunzo ya kibiashara iliyoandaliwa na shirika hilo, ameisifia hazina ya Jasiri  akisema kuwa imewasaidia pakubwa kujiendeleza kiuchumi  kutokana na mikopo inayotolewa na hazina hiyo.

Wakati huo huo amewahimiza akina mama wanaopitia dhulma za kijinsia kwenye jamii kujitokeza na kuripoti dhulma wanazopitia katika vituo vya polisi vilivyo karibu nao ili haki itendeke.

Kauli yake imepigwa jeki na Moses Okello afisa wa mipango kutoka shirika la Crew ambaye amebainisha kuwa akina mama kutoka maeneo bunge yote sita  ya kaunti ya Mombasa wananufaika kupitia hazina ya jasiri Fund ambayo kiwango chake cha riba kiko chini ikilinganishwa na mikopo inayotolewa na taasisi  nyengine.

 

Kadhalika Joseph ameirai serikali ya kaunti ya Mombasa kupitia  idara ya jinsia kuazisha miradi kama hiyo ili kuwezesha akina mama na wahanga wa dhulma za kijinsia kwa ujumla kujiimarisha kiuchumi sawia na kushirikiana kikamilifu na mashirika ya kijamii ili kuimarisha vita dhidi ya dhulma za kijinsia kwenye kaunti hiyo.