Washikadau wa elimu kaunti ya Tana River watakiwa washirikiane.
Washikadau wote wa sekta ya elimu huko kaunti ya Tana River wametakiwa washirikiane na waajibike vilivyo ili kuboresha matokeo ya mitihani ya kitaifa katika kaunti hiyo.
Akihutubia mkutano wa hadhara katika kituo cha biashara cha Garsen katika kaunti hiyo, mbunge wa Garsen Ibrahim Sane amelalamika vikali kudorora kwa viwango vya elimu katika kaunti hiyo na akaongeza kuwa sharti washikadau wa elimu wafanye kazi pamoja ili elimu iweze kuimarika vilivyo kama kaunti nyenginezo nchini.
Sane amesema kuwa kaunti hiyo ilifanya vibaya sana katika mitihani ya kitaifa ya darasa la nane na kidato cha nne ya mwaka jana 2013 huku akiongeza kuwa kwenye mtihani wa darasa la nane kaunti hiyo iliorodheshwa nambari 45 nchini kati ya kaunti 47 za humu nchini na hali mtihani wa kidato cha nne iliorodheshwa nambari 47 ya mwisho.
Na Juma Kahindi