Mtoto mwenye risasi kichwani asafirishwa hadi Nairobi kwa upasuaji
Mtoto Satrin Osinya ambaye ana risasi kichwani kufuatia shambulizi la kanisa la Likoni amesafirishwa Jumanne hadi Nairobi ambako anatarajiwa kufanyiwa upasuaji ili risasi hiyo iweze kutolewa.
Mtoto huyo wa umri wa mwaka mmoja na nusu amekuwa katika hospitali ya Makadara Mombasa hadi hapo jana ambako alihamishiwa hospitali ya Mombasa Hospital.
Shirika la madaktari wa kimataifa AMREF limefadhili ndege maalum ya kimatibabu ili kumsafirisha mtoto huyo hadi Nairobi.
Waziri wa afya James Macharia jana alitangaza kuwa serikali itasimamia matibabu ya mtoto huyo ambaye mamake alifariki wakati wa tukio hilo la siku mbili zilizopita.