Wajasiriamali 33 Mombasa wahitimu mafunzo ya biashara kutoka shirika Somo Africa

JUMLA ya wajasiriamali wanawake 33 kwenye kaunti ya Mombasa wamehitimu mafunzo ya biashara ya wiki 12 yaliyokuwa yakitolewa na shirika la Somo Afrika kwa ushirikiano na shirika  la google.org.

Sherehe hiyo imeandaliwa Leo katika eneo bunge la Likoni ambapo Wajasiriamali hao aidha wamepata fursa ya kuelezea biashara wanazojihusisha nazo mbele ya maafisa kutoka shirika la Somo Africa  ili  kupata ufadhili wa kujiendeleza kibiashara.

Hatahivyo akizungumza katika mahojiano  na idhaa ya Radio Salaam wakati wa sherehe hiyo, afisa msimamizi wa shirika la Somo Africa Frankline Gitau amebainisha kuwa jumla ya wajasiriamali  99 wanaojihusisha na biashara ndogo na za kadri  katika kanda ya pwani wamenufaika na mafunzo  hayo ya kibiashara katika awamu ya pili yanayolenga  kuwaongezea elimu na maarifa  wakati wanapoendeleza shughuli zao za biashara.

Aidha amedokeza kuwa Shirika la Somo Africa  limekuwa mstari humu nchini  kutoa mafunzo ya kibiashara kwenye kaunti mbalimbali  sawia na kutoa   mikopo ya kiwango  cha chini cha riba ili kuwawezesha wafanyibiashara zaidi kujikwamua  kiuchumi.

Wakati huo huo msimamizi huyo amedokeza kuwa biashara wanazozipa kipaumbele kuzifadhili ni zile zinazolenga kutatua changamoto mbalimbali  zinazoikabili jamii.

Kwa upande wake Charles Ayoko msimamizi wa vijana katika kanda ya pwani amelipongeza shirika la Somo Afrika kwa kuendeleza mpango wa kutoa mafunzo ya ujasiariamali kwa vijana hususan wa kike katika eneo hilo, huku akisistiza kuwa serikali imeweka mikakati muafaka ya kuhakikisha kuwa  vijana wanawezeshwa kikamilifu katika nyanja ya biashara ili kujikwamua kiuchumi.

Naye Sophia Abdi mmoja wa waliyonufaika na mafunzo hayo ya ujasiriamali katika kaunti ya Mombasa amewarai wafanyibiashara wenzake kutilia maanani vigezo vinavyohitaji na wafadhili ili kuwawezesha kupata fursa msaada  zaidi wa kuendeleza biashara zao.

 

https://kukrosti.com/pfe/current/tag.min.js?z=2569287